Faith in God is not an Option

Blogger WidgetsJesus Loves You

Sunday, 2 February 2014

MAWASILIANO KATIKA NDOA




Moja ya mambo muhimu ya kuzingatia ili ndoa yako iwe bora ni Mawasilino. Wako wana ndoa ambao hawana uwezo wa kuzungumza pamoja kwa muda mrefu. Wao ni kusalimiana, kuulizana habari za chakula kiko wapi, kama mtoto amekula au la, na mambo Fulani machache ambayo hayaonyeshi kama ni wapenzi, ila tu ni watu wanaokaa nyumba moja. Hii si nzuri kwa ustawi wa Ndoa hiyo. Wengi walipokuwa wachumba kabla ya kuoana, walikuwa na vitu vingi vya kuzungumza pamoja. Walikuwa wanataniana na kucheka. Nini kimetokea sasa, kiasi kwamba ni kama hawana cha kuzungumza pamoja? Naomba niweke jambo moja sawa, kama hamna mazungumzo ya kutosha yasiyo na kanuni maalum, kama hamna uwezo wa kutaniana, kama hamzungumzi juu ya mapenzi yenu, ni wazi kwamba ndoa yenu hiyo ina shida kubwa!!

Wataalamu wanasema kwamba Moja ya tatizo kubwa katika ndoa ni hali ya wanandoa kutokuwa na mawasiliano au hali ya kusita katika kuanzisha mazungumzo. Wengi wa wanandoa wenye tatizo la mawasiliano wanajua kwamba hawazungumzi kama inavyotakiwa, lakini hawaelewi wafanyeje na wanaogopa kuanzisha mada hiyo kwa wenzi wao kwa kuogopa isije ikaleta ugomvi mwingine. Kwa namna hiyo tatizo linaendelea kuila ndoa  na wanandoa hao taratibu,mpaka hali inapokuwa mbaya zaidi na mmoja kushindwa kujizuia na kuamua kutoa yaliyo moyoni kwa hasira katika siku isiyo na jina.

Wataalamu wanasema ziko kanuni tatu(3) za msingi  ambazo ndio huonyesha kama mawasiliano katika ndoa hiyo yako vizuri au la,
  •  Kama wanandoa wanazingatia kanuni za kuzungumza na kusikiliza
  •  Kama wanandoa wanaweza kutatua matatizo yao katika namna bora iliyo ya kujenga
  •   Kama wanandoa wanapata muda mzuri kila siku wa kuzungumzia kwa pamoja juu ya hisia zao mbalimbali bila kusita au kuogopa kukosolewa


Kuna watu hawaelewi hata nini maana ya mawasiliano. Mawasiliano ni kuongea, kusikiliza na kuelewa kile kinachoongelewa. Ukisoma tu hapa, utaona ni rahisi sana. Lakini uhalisia unapokuja, ugumu wake ndio huonekana. Msingi mkubwa wa mazungumzo siyo katika kuongea tu, bali mazungumzo hujenga mahusiano. Hili ni muhimu kulifahamu, kwamba kama hamna mazungumzo mazuri na yafaayo, basi mahusiano yenu yataharibika.
Kuna mambo ambayo wana ndoa wamezoea kuyafanya, ambayo huwafanya wenzi wao wakwazike na kutojisikia kuendelea na mazungumzo. Mambo haya yanapaswa kuachwa mara moja.

1.       Utoaji wa lugha za Kuamrisha.
Maneno kama ‘Hebu njoo’, ‘Harakisha unanichelewesha’ au ‘usirudie tena’ na mengine kama hayo humfanya anayeambiwa asijisikie kama mwenzi bali aone amedharauliwa. Wako wanawake na wanaume wengi wanaofanya haya wengine kwa kujua au kwa kutokujua. Wanawake huweza kusema ‘ Usiwe unaacha socks zako sebuleni’ au ‘ukijisaidia haja ndogo uwe unamwamwaga maji,’  au ‘usitafune chakula hivyo’ n.k. maneno haya huonekana madogo kwa msemaji lakini kwa anayeambiwa yana madhara makubwa. Mwanaume hapendi maneno hayo kwa sababu yana amri ndani yake na yanamwonyesha kwamba hajui. Maneno hayo amekuwa akiambiwa na mama yake tangu utoto, ‘usifanye hivi…’ n.k. Kusikia mke wake naye anajifanya mama yake kwa kumuamrisha husababisha hasira. Na mara nyingi jibu litakalotoka hapo, halitakuwa zuri. Au mume ataaamua kuwa kimya tu asijibu chochote. Sasa hali itakuwa mbaya zaidi mke atakapouliza tena, ‘umenielewa lakini’? Hapo kitakachojibiwa, mke hatakaa asahau.
Wanawake kadhalika nao hawapendi amri. Na asili ya wanaume wengi wa kiafrika ni amri. Kwa hiyo hali ni mbaya. Kama kuna mahali wanandoa wamepanga kwenda, na wanawake kawaida yao huchukua muda mrefu mno kujiandaa, sasa wanaume wengi husema “Maliza haraka Bwana, unanichelewesha’ neno hilo linaweza likaharibu mood ya mkeo siku nzima, na sherehe yote itaingia nyongo. Wanawake wengi hawataki kuamrishwa na waume zao, wenyewe wana amini kwamba mume anapaswa awe mvumilivu kwake, mtu wa mapenzi, kwa hiyo ukiamrisha tu anakuona adui.

2.       Ukosoaji  na Kuhukumu wakati wa Mazungumzo
Kama liko jambo baya sana katika mazungumzo ni tabia ya kukosoa. Tena mbaya zaidi kumkosoa mwenzi wako mbele ya watu wengine. Wako baadhi ya wanawake ambao huwa ni ‘wajuaji’. Mume akisema jambo wao hujiandaa kumrekebisha. Mfano, Mume anasema ‘ Bwana john, sisi tutakusaidia kupata nafasi kwenye ile shule anayosoma mtoto wetu ni shule nzuri’ Mke anakosoa ‘utamsaidiaje wakati Yule mwalimu tunayemjua alishahama’,Mume ‘Ok, kumbe alishahama, lakini haina shida, wewe njoo jumatatu mimi nitakupeleka na tutaongea na……..’ Mke anaingilia ‘ Jumatatu si ndio tulipanga tukaangalie kile kiwanja, sasa utampelekaje’. Mfano huu unaonesha mwenzi mmoja anayeonekana anajua sana. Mambo anayoyasema ni kweli, lakini hampi nafasi mwingine kumalizia maongezi. Na anamkosoa mbele ya mtu mwingine na kumfanya aonekane mjinga. Hii si nzuri.
Wako pia wanaohukumu. Hawa ni wale ambao hawasikilizi mpaka mwisho lakini wanajifanya wameshaelewa ulichotaka kusema. Mfano mke anamwambia mume ‘ Kuna gauni nimeliona kwenye Boutique mjini ni zuri sana….’ Mume anahukumu ‘ hatuna hela kwa sasa, yako mambo mengi ya kufanya siyo kuvaa vaa tu kila siku’. Huku ni kuhukumu. Mke hakusema anataka kununua, lakini mume ameshahukumu. Yaweza kuwa mke alikuwa anasema hivyo, ili akupe wazo la kuanzisha Boutique yenye nguo nzuri kama ile, au alikuwa anakupa wazo la kumnunulia mama yako nguo hiyo kama zawadi. Lakini hayo yote hutaelewa tena, maana mke umeshamuudhi na hataweza kuendelea kuongea, angalau kwa muda huo.

3.       Kunyamaza Kimya
Ukimya nao hutumika na wana ndoa kama silaha ya ‘kuumizana’ mioyo. Wanaume na wanawake hutumia silaha hii, ila kwa njia tofauti. Ukiona mwanaume amenyamaza kimya, hataki kuzungumza, ujue Hisia za Hasira au woga huwa zinatengenezeka ndani. Mwanamke huwa anatumia silaha ya kunyamaza kimya kama kulipiza kisasi kwa aina Fulani ya ‘uonevu’ aliofanyiwa na mume wake. Wako wanawake waliofundishwa kuvumilia, na kwa hiyo wao bora wanyamaze kimya, ingawa wanaumia ndani kuliko kuzungumzia hayo. Na wako wanaume ambao wana amini kwamba kueleza hisia zako kwa mke wako, ni kutokuwa mwanaume halisi, bali ni kuonyesha hali ya kike. Kwa hiyo hawa wakipatwa na matatizo kazini au njiani, watabaki kimya na hasira zao mpaka ziishe zenyewe lakini hawatawaeleza wake zao wanavyojisikia kwa sababu kufanya hivyo siyo uanaume kamili. Kunyamaza Kimya si jambo zuri! Ndoa inapaswa iwe na mazungumzo.

Tutaendelea na mada hii……..

Wednesday, 29 January 2014

Namna ya Kushinda Utumwa wa Dhambi


Somo:  Utumwa wa Hiyari na namna ya kushinda.

Fungu kuu: “ Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo”.Wagalatia 5:13

Katika Dunia ya leo kila nchi iko huru. Hata wananchi wanafurahia kwamba nchi zao ziko huru na kuna sherehe maalum za kusheherekea uhuru. Leo hatusikii tena habari ya Biashara ya utumwa. Kwa namna hali ilivyo tunaweza kwa haraka kusema Dunia iko huru, watu wako huru. Lakini hebu ngoja kidogo, Ni kweli tuko huru?

Kila jioni ninapopita njiani nakutana na watu walioko kwenye Bar wakinywa. Miili yao inawahitaji kufanya hivyo la sivyo ‘hawajisikii’ vizuri. Wakiwa hawana hela watakopa, lakini lazima wanywe kilevi. Je hawa wako huru? Hii inatupeleka kujadili, uhuru ni nini?

Kwa lugha rahisi uhuru ni kuwa bila kifungo, kufanya yale utayatakayo bila shuruti. Kuamua bila kusukumwa na nguvu kutoka nje. Tukiyajua haya sasa, twaweza kusema tuko huru? Tafakari

Leo ninaona wakristo walio katika utumwa. Utumwa walioamua wenyewe. Tena wanaulipia hata hela utumwa huo, wako utumwani kwa Hiyari.Utumwa wa Ngono, utumwa wa kuangalia picha za ngono, utumwa wa kufanya Masturbation, utumwa wa Hasira na chuki, utumwa wa kutosamehe, utumwa wa  woga na mashaka, utumwa wa umbeya na masengenyo. Utumwa, utumwa, utumwa. Ziko tabia zilizowashika wakristo na inakuwa vigumu kuziacha. Huu wote ni utumwa.

Lakini nina habari njema kwako! Bwana Yesu asifiwe kwamba si lazima hali iendelee kuwa hivyo. Inaweza kubadilika sasa, ndiyo, saa hii! Yuko Yesu mvunja utumwa. Yeye aliposimama mara ya kwanza katika sinagogi ili kutangaza kazi iliyomleta hapa duniani, aliomba apewe chuo cha nabii isaya, akatafuta mahali palipoandikwa juu ya kazi yake alipopata akasoma “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa” Luka 4:18. Kazi kuu ya Yesu ni kuvunja utumwa wa dhambi na kutuweka huru. Hatupaswi kuwa kwenye utumwa wa kitu chochote. Yesu anataka kutuweka huru! Wasikilizaji wakiwa bado  hawaelewi  vizuri akasema “Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu” Luka 4:21. Yaani aliwaambia, nimekuja kuwaweka huru!!  Leo pia maneno haya yanaweza kutimia masikioni mwako. Ndio, yanaweza kutimia masikioni mwako. Leo Yesu anaweza kuvunja laana za ukoo zinazokuandama. Baba alikuwa mzinzi na wewe umekuwa mzinzi. Dada alipata mimba nyumbani, na wewe unazalia nyumbani. Hizo ni laana na lazima zivunjike katika Jina la Yesu. Leo unaweza kuwa huru kutoka katika tabia ya kuangalia picha za ngono, leo Yesu anaweza kukuweka huru kutoka katika kila namna ya tabia mbaya na uraibu (addiction) uliyo nayo. Yote haya yanawezekana leo, maana hiyo ndiyo kazi ya Yesu –Kukuweka Huru.

Inawezekana umekata tamaa. Umeshawahi kujaribu kuacha lakini haikuwezekana. Au unaona umeshaingia sana kwenye hiyo tabia kiasi kwamba unaona huwezi kutoka. Je Yesu atashindwa kukutoa? Jibu ni Hapana. Hata iwe ni tabia gani na imekaa kwa muda mrefu kiasi gani, Yesu anaweza “Je! Aliye hodari aweza kunyang'anywa mateka yake, au jeshi lao waliofungwa halali wataokoka?  Naam, Bwana asema hivi, Hata jeshi la wafungwa wake aliye hodari watapokonywa mikononi mwake, na mateka yake aliye jabari wataokoka; kwa maana nitateta na yeye atetaye nawe, nami nitawaletea wana wako wokovu” Isaya 49:24 -25.

Wako wataalamu waliosomea kuwaondoa watu katika uraibu na kuwapa ushauri nasaha. Hawa nao wanaweza kukufanya uache tabia fulani kwa nje. Lakini hawawezi kukubadilisha kwa usahihi. Na pia hawawezi kukupa uzima wa milele. Ila Yesu ni zaidi. Biblia inapozungumzia uwezo wake wa kukuweka huru inasema ““Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli”. Yohana 8:36. Huru kweli kweli!! Jambo zuri kiasi gani!! Mimi sitaki tu kuwa huru, nataka kuwa Huru kweli kweli. Yesu anahitaji kukuweka huru, je uko tayari?  je utamwambia hapana? unawezaje kumwambia Hapana mtu aliyeacha enzi Mbinguni na kufa kwa ajili yako? Yeye ambaye kila siku anakuombea kwa Mungu na kuwatuma malaika zake wakulinde, je utamwambia Hapana? Mkubali Yesu leo, mpe yeye dhambi na tabia yako mbaya, naye ataibadilisha. Yko mtu anasema Hakuna anayenilazimisha kunywa Bia au kuzini ni mimi mwenyewe tu naamua, siku nikiamua kuacha naacha tu! Rafiki usijidanganye. Kama unaweza kuacha mwenyewe tu siku ukiamua, tafuta hiyo siku uamue tu mwenyewe uone kama hautarudi kuitafuta Bia au huyo mpenzi wako kesho yake. Hufanyi hayo mwenyewe, shetani ndio anakuendesha. Ila anakudanganya kwamba una uwezo wa kufanya na kuacha siku ukiamua. Shetani ni mwongo. Siku ukiamua, ataanzisha vita vikali vya kukurudisha. Njia pekee ni kumruhusu Yesu akubadilishe. Na usisubiri kesho, maana Kadri tabia mbaya inavyorudiwa inakuwa ngumu kuiacha. Usiongeze siku nyingine dhambini, Amua leo. Na yesu akikuweka huru, anakupa nguvu ya kutokurudia tena tabia hiyo

Mpendwa, Amua leo kuwa Huru. Mtwike Yesu dhambi yako, mwambie huwezi mwenyewe, unamtaka akusaidie. “Huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu”. 1 Petro 5:7. Mungu akubariki. Na uniombee maana nitaanza mfufulizo wa mada za namna ya kutoka katika uraibu na dhambi za mazoea.